Language 

Our Lady of Medjugorje Messages containing 'yeye'

Total found: 72
Wanangu wapendwa, nawashukuru kwa kuitikia miito yangu na kukusanyika karibu nami, Mama yenu wa mbinguni. Najua kwamba mnanifikiri kwa upendo na matumaini. Mimi ninawapendeni nyote kama vile anavyowapendeni Mwanangu ambaye, kwa upendo wake wenye huruma, ananituma nije kwenu, mara nyingi pia. Yeye, aliyekuwa mtu na aliye Mungu, Mmoja na Utatu; Yeye aliyeteswa kwa ajili yenu mwilini na nafsini. Yeye aliyejifanya Mkate ailishe nafsi zenu na hivyo kuziokoa. Wanangu, nawafundisha jinsi ya kustahili upendo wake, kumwelekeza mawazo yenu, kumwishi Mwanangu. Mitume wa upendo wangu, ninawafunika kwa joho langu kwa sababu, kama Mama yenu, nataka kuwalinda. Nawasihi: mwuombee ulimwengu wote: moyo wangu unateswa. Dhambi zinaongezeka, ni nyingi mno. Lakini kwa msaada wenu – mlio wanyenyekevu, wanyofu, wenye upendo, watawa na watakatifu – moyo wangu utashinda. Mpendeni Mwanangu kupita wote na ulimwengu wote kwa njia yake. Msisahau kabisa ya kuwa kila ndugu yenu ana ndani yake kitu cha thamani: nafsi. Kwa hiyo, wanangu, pendeni wale wote wasiomjua Mwanangu ili kwa njia ya maombi na upendo utokao katika maombi, wawe wema zaidi. Ili wema uweze kushinda ndani yao. Ili nafsi zao ziweze kuokoka na kupata uzima wa milele. Enyi mitume wangu, wanangu. Mwanangu aliwaambieni mpendane. Hiyo iandikwe mioyoni mwenu na kwa kusali jaribuni kuishi upendo huu. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, kwa mapenzi ya Baba wa mbinguni, kama Mama wa Yule anayewapendeni, nipo hapa pamoja nanyi niwasaidieni kumjua, kumfuata. Mwanangu amewaachieni nyayo za hatua zake, ili iwe rahisi zaidi kwenu kumfuata. Msiogope, msiwe na wasiwasi. Mimi nipo pamoja nanyi! Msichoke, maana sala nyingi na sadaka zinahitajiwa kuwasaidia wale wasiomwomba, wasiompenda na wasiomjua Mwanangu. Muwasaidie mkiona ndani yao ndugu zenu. Enyi mitume wa upendo wangu, sikilizeni sauti yangu ndani yenu, hisieni upendo wangu. Kwa hiyo salini: salini mkitenda, salini mkitoa. Salini kwa upendo, salini kwa matendo na kwa fikira, kwa jina la Mwanangu. Kadiri mtakavyotoa upendo, ndivyo mtakavyoupokea. Upendo utokao katika Upendo huangaza ulimwengu. Ukombozi ni upendo, na upendo hauna mwisho. Wakati Mwanangu atakapokuja tena duniani, atatafuta upendo katika mioyo yenu. Wanangu, Yeye alifanya kwa ajili yenu matendo mengi ya upendo. Ninawafundisha kuyaona, kuyaelewa na kumshukuru mkimpenda na kumsamehe sikuzote na tena jirani yako. Kwa kuwa kumpenda Mwanangu maana yake ni kusamehe. Mwanangu hapendwi, ikiwa hatuwezi kumsamehe jirani yetu, ikiwa hatuwezi kumwelewa jirani yetu, ikiwa tunamhukumu. Wanangu, faida gani kusali, msipopenda wala msiposamehe? Nawashukuru.
Wanangu wapendwa! leo ninawaalika kuwa watu wa sala. Salini mpaka hata sala itakapokuwa kwenu furaha na mkutano na Yeye aliye juu. Yeye atageuza moyo wenu nanyi mtakuwa watu wa upendo na wa amani. Wanangu, msisahau kwamba shetani ni mwenye nguvu na anataka kuwaachisha kusali. Ninyi, msisahau kwamba sala ni kifunguo cha siri cha mkutano pamoja na Mungu. Kwa hiyo Mimi nipo pamoja nanyi, niwaongoze. Msiache kusali. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa, nikiwatazama hapa mmekusanyika kunizunguka, Mama yenu, ninaona nafsi safi nyingi. Ninawaona wanangu wengi wanaotafuta upendo na faraja lakini hakuna mtu anayewapa. Ninawaona hata wale wanaotenda mabaya maana hawana mifano myema, maana hawajamjua mwanangu. Mwanangu anawatuma ninyi kwangu, Mama, sawa kwa wote, niwafundisheni kupenda, ili muelewe ya kuwa ninyi ni ndugu. Ninatamani kuwasaidia. Mitume wa upendo wangu, kwa mwanangu yamtosha tamaa hai ya imani na upendo na atayakubali, lakini mnapaswa kustahili, kuwa na tamaa na mioyo wazi, Mwanangu huingia katika mioyo wazi. Mimi kama Mama ninatamani kwamba mjue Mwanangu katika kweli: Mungu aliyezaliwa na Mungu, kwamba mjue ukuu wa Upendo wake, ambao mnahitaji. Yeye amezichukua juu yake dhambi zenu, ameupata Ukombozi wenu, na badala yake anaomba mpendane ninyi kwa ninyi. Mwanangu ni upendo, Yeye anawapenda watu wote bila tofauti, watu wote wa nchi zote, wa mataifa yote. Ikiwa ninyi, wanangu, mngeishi upendo wa Mwanangu, ufalme wake ungekwisha kuwa duniani. Kwa hiyo, Mitume wa upendo wangu, salini, salini ili Mwanangu na upendo wake wawe ndani yenu nanyi muweze kuwa mfano wa upendo na muweze kuwasaidia wote wale ambao hawajamjua Mwanangu. Msisahau kamwe kwamba Mwanangu, mmoja na utatu, anawapendeni. Pendeni na wombeeni wachungaji wenu. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa! Katika kipindi hiki cha neema ninawaalika kusali. Salini na tafuteni amani, wanangu. Yeye aliyekuja hapa duniani awatoe amani, pasipo kuwabagua kuwa ninyi ni nani na ni kitu gani - Yeye, Mwanangu, ndugu yenu, kwa njia yangu anawaalika kuongoka maana pasipo Mungu hamna baadaye wala uzima wa milele. Kwa hiyo aminini, salini na isheni katika neema na mkingojea mkutano wenu wa binafsi pamoja naye. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa! Katika kipindi hiki cha neema ninawaalika nyote kujifungua na kuishi amri ambazo Mungu aliwapeni ili, kwa njia ya sakramenti, ziwaongoze katika njia ya wongofu. Ulimwengu na vishawishi vya ulimwengu vinawajaribu; ninyi, wanangu, angalieni viumbe vya Mungu ambavyo katika uzuri na unyenyekevu Yeye aliwapa, na mpendeni Mungu, enyi wanangu, kuliko kila kitu naye atawaongoza katika njia ya wokovu. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa, Mwanangu, aliye mwanga wa upendo, yote aliyoyafanya na anayoyafanya hufanya kwa ajili ya upendo. Vivyo hivyo nanyi, wanangu, mnapoishi katika upendo, mnapompenda jirani yenu na mnapofanya mapenzi yake. Enyi mitume wa upendo wangu, jifanyeni wadogo! Mfungulieni Mwanangu mioyo yenu safi, ili Yeye aweze kutenda kazi kwa njia yenu. Kwa msaada wa imani, mjijazie upendo. Lakini, wanangu, msisahau ya kuwa Ekaristi ndiyo kiini cha imani. Yeye ndiye Mwanangu anayewalisheni kwa Mwili wake na kuwaimarisheni kwa Damu yake. Yeye ndiye ajabu ya upendo: Mwanangu ajaye tena mwenye uhai ili kuzifufua nafsi. Wanangu, mkiishi katika upendo, ninyi mnafanya mapenzi ya Mwanangu naye huishi ndani yenu. Wanangu, matakwa yangu ya kimama ni kwamba mpendeni zaidi na zaidi, maana Yeye anawapenda kwa upendo wake. Anawapa upendo wake ili muweze kuueneza kwa watu wote kandokando yenu. Kwa njia ya upendo wake, kama mama mimi nipo pamoja nanyi kuwaambieni maneno ya upendo na matumaini, kuwaambieni maneno ya milele na ya kushinda wakati na mauti, kuwaalikeni kuwa mitume wangu wa upendo. Nawashukuru!
Wanangu wapendwa, katika wakati huo wa wasiwasi ninawaalika kumwamini zaidi Mungu aliye Baba yenu mbinguni na anayenituma kuwaongozeni kwake. Ninyi, mfungulieni mioyo yenu kwa zawadi ambazo Yeye ataka kuwapeni na katika kimya ya moyo wenu mwabuduni Mwanangu, aliyetolea maisha Yake ili muishi katika milele anakotaka kuwaongoza. Matumaini yenu na yawe furaha ya kukutana na Yule Aliye juu katika maisha ya kila siku. Kwa hiyo ninawaalika: msiache sala maana sala hutenda miujiza. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa! Hii ni siku ambayo Bwana amenipa kwa kumshukuru kwa kila mmoja wenu, kwa wale walioongoka na waliokubali habari zangu na walioshika njia ya wongofu na ya utakatifu. Wanangu, furahini, maana Mungu ni mwenye rehema na anawapenda wote kwa Upendo wake mkubwa sana na kuwaongoza kuelekea njia ya wokovu kwa msaada wa kuja kwangu hapa. Mimi ninawapenda wote na ninawapa mwanangu ili Yeye awape amani. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa, Mimi ni Mama wa ninyi nyote na kwa hiyo msiogope kwa sababu mimi ninasikia sala zenu, najua kwamba mnanitafuta na kwa hiyo ninamwomba Mwanangu kwa ajili yenu; Mwanangu ambaye yu katika mwuungo pamoja na Baba wa mbinguni na pamoja na Roho Mfariji, Mwanangu anayewaongoza roho katika Ufalme alikotoka, ambao ni Ufalme wa amani na wa mwanga. Wanangu, mmepewa uhuru wa kuchagua, kwa hiyo mimi kama Mama ninawasihi mchague uhuru kwa mema, na kwa moyo safi na mnyofu mnaelewa, ingawa pengine hamwelewi maneno yote, ndani yenu mng'amue ukweli ni nini. Wanangu, msipoteze ukweli na maisha ya kweli kwa kufuata maneno ya uongo. Kwa njia ya maisha ya kweli Ufalme wa mbinguni huingia katika mioyo yenu, ni Ufalme wa upendo, wa amani na wa maelewano. Katika Ufalme ule, wanangu, hautakuwa na ubinafsi wa kuwaondoa kutoka kwa Mwanangu, kutakuwa na upendo na maelewano na jirani yako. Kwa hiyo kumbukeni, ninawaambieni tena, kusali maana yake ni kuwapenda wengine, kumpenda jirani yako, kujitoa kwa ajili yao; pendeni na toeni kwa jina la Mwanangu, hapo Yeye atatenda kazi ndani yenu na kwa ajili yenu. Wanangu, fikirini daima juu ya Mwanangu, mpendeni bila kipimo na hapo mtakuwa na maisha ya kweli, yatakayokuwa ya milele. Nawashukuru enyi Mitume wa upendo wangu!
Wanangu wapendwa! Mungu aliniita ili niwaongozeni kwake, maana Yeye ndiye nguvu yenu. Kwa hiyo ninawaalika kumwomba na kumtegemea, maana Yeye ndiye kimbizo lenu kutoka kila uovu uliokaribu na kupeleka mioyo mbali kutoka neema na furaha mnakoitwa. Wanangu isheni Mbingu hapa duniani ili mkae vizuri na amri za Mungu ziwe mwanga katika njia yenu. Mimi nipo pamoja nanyi na kuwapenda nyote kwa upendo wa kimama. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa, maneno yangu ni manyofu lakini yamejaa upendo wa kimama na mahangaiko. Wanangu, juu yenu vivuli vya giza na vya udanganyifu vinaenea zaidi na zaidi, mimi ninawaiteni kuelekea mwanga na ukweli, mimi ninawaita kuelekea Mwanangu. Yeye peke yake huweza kugeuza kukata tamaa na maumivu yetu kuwa amani na utulivu, Yeye peke yake huweza kutoa matumaini katika maumivu makali sana. Mwanangu ni uzima wa ulimwengu, kwa kadiri mtakavyomjua, ndivyo mtakavyomkaribia na kumpenda maana Mwanangu ni upendo, na upendo unageuza yote. Yeye hufanya la ajabu hata neno lisilo la maana bila upendo machoni penu. Kwa hiyo nawaambieni tena ya kwamba mnapaswa kupenda sana ikiwa mnatamani kukua kiroho. Najua, enyi mitume wa upendo wangu, kwamba si rahisi sikuzote, lakini, wanangu, hata njia ngumu ni njia zinazoongoza kwenye ukuaji wa kiroho, wa kiimani na kwa Mwanangu. Wanangu, salini, mfikirie Mwanangu, nyakati zote za siku zenu inueni nafsi zenu kwake nami nitakusanya sala zenu kama maua kutoka bustani nzuri kuliko zote na kumpa Mwanangu. Muwe hakika mitume wa upendo wangu, wapeni wote upendo wa Mwanangu, muwe bustani zenye maua mazuri kuliko yote. Kwa njia ya sala saidieni wachungaji wenu ili waweze kuwa baba za kiroho waliojaa upendo kwa watu wote. Nawashukuru.
Wanangu, ninawaomba kuwa hodari wala kutowayawaya, maana hata mema madogo zaidi, ishara ya upendo mdogo zaidi hushinda maovu yanayoonekana zaidi na zaidi. Wanangu nisikilizeni ili mema yashinde, ili muweze kujua upendo wa Mwanangu ulio furaha mkubwa zaidi kuliko zote. Mikono ya mwanangu inawakumbatia, Yeye, apendaye nafsi, Yeye ambaye amejitolea kwa ajili yenu na kunajitolea sikuzote tena katika Ekaristi, Yeye aliye na maneno ya Uzima wa milele; kujua upendo wake, kufuata hatua zake, maana yake ni kuwa na mali ya kiroho. Huo ni utajiri unaojaza hisia iliyo njema, na unaoona upendo na mema popote. Mitume wa upendo wangu, wanangu, muwe kama mionzi ya jua ambayo kwa joto la upendo wa Mwanangu inawapasha joto wote wale wanaoizunguka. Wanangu, ulimwengu unahitaji mitume wa upendo, ulimwengu unahitaji sala nyingi, lakini sala zinazosaliwa kwa moyo na roho, si kwa midomo tu. Wanangu, muwe na hamu ya utakatifu mkiwa na unyenyekevu unaomwezesha Mwanangu kufanya kazi kwa njia yenu, kama Yeye apendavyo. Wanangu, sala zenu, fikira zenu na matendo yenu, haya yote yawafungulia ama kuwafungia mlango wa Ufalme wa Mbinguni. Mwanangu aliwaonyesha njia na kuwapa tumaini, mimi ninawafariji na kuwapa moyo maana, wanangu, mimi nilijua maumivu, lakini nilikuwa na imani na tumaini, sasa nimepata thawabu ya uzima katika Ufalme wa Mwanangu. Kwa hiyo, nisikilizeni, jipeni moyo, msiwayawaye. Nawashukuru.
Wanangu, Moyo wangu wa kimama unateseka wakati ninapotazama wanangu wasiopenda ukweli, wanaouficha; wakati ninapotazama wanangu wasiosali kwa moyo wala kwa matendo. Nimesikitika wakati ninapomwambia Mwanangu ya kuwa wana wangu wengi hawana imani tena, ya kuwa hawamjui Yeye, Mwanangu. Kwa hiyo ninawaalika, mitume wa upendo wangu: mjaribu kutazama mpaka ndani ya mioyo ya watu, na kule bila shaka mtapata hazina ndogo iliyofichwa. Kutazama hivyo ni rehema ya Baba wa mbinguni. Kutafuta mema hata palipo maovu makubwa zaidi, kutafuta kuwaelewana wala kutohukumiana: hilo ni neno ambalo Mwanangu anawaombeni. Nami, kama Mama, ninawaalika kumsikiliza. Wanangu, roho ni yenye nguvu kuliko mwili na, ikichukuliwa na upendo na matendo hushinda vikwazo vyote. Msisahau: Mwanangu aliwapendeni na anawapenda. Upendo wake ni pamoja nanyi na ndani yenu, wakati mpo kitu kimoja pamoja naye. Yeye ni mwanga wa ulimwengu, na hakuna mtu wala kitu kiwezacho kumsimamisha katika utukufu wa mwisho. Kwa hiyo, mitume wa upendo wangu, msiwe na hofu ya kushuhudia ukweli! Ushuhudieni kwa hamu, kwa matendo, kwa upendo, kwa sadaka yenu, lakini hasa kwa unyenyekevu. Shuhudieni ukweli kwa wale ambao hawajajua Mwanangu. Mimi nitakuwa karibu nanyi, mimi nitawatia moyo. Shuhudieni upendo usioishi tena, maana huja kutoka Baba wa mbinguni ambaye ni wa milele na anawatolea wana wangu wote umilele. Roho wa Mwanangu itakuwa karibu nanyi. Ninawaalika tena, wanangu: muwaombee wachungaji wenu, ombeni ili upendo wa Mwanangu uweze kuwaongoza. Nawashukuru.
Katika tokeo la mwisho la kila siku tarehe 12 Septemba 1998 Bikira Maria alimwambia Yakobo Kolo ya kuwa ataona tokeo mara moja kila mwaka, tarehe 25 Decemba, siku ya Noeli. Hivyo kumekuwa na tokea hata mwaka huu. Tokeo limeanza saa 7 na dakika 38 na likadumu dakika 9. Bikira Maria amekuja pamoja na Mtoto Yesu mikononi mwake. Bikira Maria kwa njia ya Yakobo alipitisha ujumbe huu:
Wanangu wapendwa, katika siku hii ya neema ninawaalika kupenda. Wanangu, Mungu anawapenda kupita kiasi na kwa hiyo wanangu, mmejaa imani, bila kutazama nyuma na bila hofu mwachieni kabisa mioyo yenu ili Mungu aijaze kwa upendo wake. Msiwe na hofu kuamini upendo Wake na rehema Yake maana upendo Wake ni mwenye nguvu kuliko kila udhaifu wenu na hofu. Kwa hiyo, wanangu, mmejaa upendo katika mioyo yenu mwamini Yesu na mseme Ndiyo yenu maana Yeye ni njia ya pekee ya kuwaongoza kwa Baba wa milele.
Wanangu wapendwa! Ninawaletea Mwanangu Yesu ambaye ni Mfalme wa amani. Yeye anawapa amani, basi amani hii isiwe yenu tu, wanangu, lakini wapelekeeni na wengine katika furaha na unyenyekevu. Mimi nipo pamoja nanyi na kuwaombeeni katika wakati huu wa neema ambayo Mungu anataka kuwapa. Uwepo wangu ni ishara ya upendo, wakati nipo hapa pamoja nanyi niwalinde na kuwaongoza kuelekea umilele. Asanteni kwa kuitikia wito wangu.
Wanangu wapendwa, inasikitisha kwamba katikati yenu, wanangu, yapo mashindano mengi, chuki, masilahi yenu wenyewe na ubinafsi. Wanangu, hivi kwa urahisi mnamsahau Mwanangu, maneno Yake na upendo Wake. Imani inazimika katika roho nyingi na mioyo imetekwa na vitu vya ulimwenguni. Lakini moyo wangu wa kimama unajua ya kuwa katikati yenu kuna wale wanaoamini na kupenda, wale ambao wanajaribu kumkaribia Mwanangu zaidi na zaidi, ambao wanamtafuta bila kuchoka na namna hii, wananitafuta hata mimi. Hawa ndio wanyenyekevu na wapole ambao, pamoja na maumivu na mateso wanayoyachukua katika kimya, pamoja na tumaini lao na hasa pamoja na imani yao, ni mitume wa upendo wangu. Wanangu, mitume wa upendo wangu, ninawafundisha ya kuwa Mwanangu hatafuti sala tu pasipo kuchoka bali hata matendo na hisia. Salini ili katika sala mpate kuzidi katika imani na katika upendo. Mpendane wenyewe kwa wenyewe: hilo ndilo analotaka Yeye, hiyo ndiyo ni njia ya uzima wa milele. Wanangu, msisahau ya kuwa Mwanangu ameleta mwanga kwa ulimwengu huu. Ameuleta kwa wale ambao walitaka kuuona na kuupokea. Hawa muwe ninyi, maana huu ndio mwanga wa ukweli, wa amani na wa upendo. Mimi ninawaongoza kama mama kumwabudu Mwanangu, kumpenda pamoja nami. Fikira zenu, maneno na matendo yenu yamwelekee Mwanangu, yawe katika jina Lake: hapo tu moyo wangu utajazwa. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, upendo na wema wa Baba wa mbinguni yanatoa mafunuo ili kwamba imani ikue, iweze kuelezwa, ilete amani, salama na matumaini. Hivi mimi nami, wanangu, kwa ajili ya upendo wenye rehema wa Baba wa mbinguni ninawaonyesha sikuzote tena njia ya kwenda kwa Mwanangu, kwa wokovu wa milele; kwa bahati mbaya, lakini, wanangu wengi hawataki kunisikiliza. Wanangu wengi wanasita. Lakini mimi, mimi, katika wakati na zaidi ya wakati, sikuzote nimemtukuza Bwana kwa mambo yale yote aliyoyatenda ndani yangu na kwa njia yangu. Mwanangu anajitolea kwenu, anamega mkate pamoja nanyi, anawaambieni maneno ya uzima wa milele ili muweze kuwaletea watu wote. Nanyi, wanangu, mitume wa upendo wangu, mnaogopa nini, ikiwa Mwanangu ni pamoja nanyi? Mwonyesheni nafsi zenu, ili Yeye aweze kuwa ndani yao na aweze kuwafanyeni kuwa vyombo vya imani, vyombo vya upendo. Wanangu, ishini Injili, ishini upendo wenye rehema kuelekea mwenzenu; lakini hasa ishini upendo kuelekea Baba wa mbinguni. Wanangu, hamkuungana kwa bahati tu. Baba wa mbinguni haunganishi watu kwa bahati tu. Mwanangu anaongea na nafsi zenu, nami ninaongea moyoni mwenu. Kama Mama ninawaambia: tembeeni nami! Pendaneni, na kutoa shuhuda! Hampasi kuogopa kulinda Ukweli, ambao ni Neno la Mungu, lililo la milele na lisilogeuka kamwe, kwa mifano yenu. Wanangu, yule anayetenda kazi katika mwanga wa upendo wenye rehema na ukweli, anasaidiwa sikuzote na Mbingu na hayuko peke yake. Mitume wa upendo wangu, waweze kuwatambua sikuzote katikati ya wengine wote katika maficho, upendo na utulivu wenu. Mimi nipo pamoja nanyi. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, ninawaita mitume wa upendo wangu. Ninawaonyesha Mwanangu, aliye amani ya kweli na upendo wa kweli. Kama Mama, kwa ajili ya neema ya kimungu, ninatamani kuwaongoza kwendea Yeye. Wanangu, kwa hiyo ninawaalika kujitazama ninyi wenyewe mkianzia kwa Mwanangu, kumtazama kwa moyo na kuona kwa moyo mahali mlipo na maisha yenu yanakwenda wapi. Wanangu, ninawaalika kuelewa ya kuwa mnaishi kwa ajili ya Mwanangu, kwa njia ya upendo wake na sadaka yake. Ninyi mnamwomba Mwanangu kuwa mwenye rehema nanyi, lakini mimi ninawaalika ninyi kuwa na rehema. Mnamwomba kuwa mwema nanyi na kuwasamehe, lakini tangu lini mimi ninawasihi ninyi, wanangu, kusamehe na kupenda watu wote mnaokutana nao! Mtakapoelewa kwa moyo maneno yangu, mtaelewa na kujua upendo wa kweli, na mtaweza kuwa mitume wa upendo ule, enyi mitume wangu, wanangu wapendwa. Nawashukuru.
Wanangu wapendwa, kama Mama ambaye anajua wana wake, ninajua ya kuwa mnamtamani Mwanangu. Ninajua ya kuwa mnatamani ukweli, amani, na kilicho chema wala si uovu. Kwa sababu hiyo mimi, kama Mama, kwa njia ya upendo wa Mungu ninawaita ninyi na kuwaalika ili, mkisali kwa moyo safi na wazi, mmtambue ninyi wenyewe Mwanangu, upendo wake, na Moyo wake wenye rehema. Mwanangu alikuwa akiona uzuri katika vitu vyote. Yeye anatafuta mema, hata yale mema madogo yanayofichika, katika roho zote, ili kusamehe maovu. Kwa hiyo, wanangu, mitume wa upendo wangu, ninawaalika kumwabudu, kumshukuru daima na kumstahili. Maana yeye aliwaambieni maneno ya kimungu, maneno ya Mungu, maneno yaliyo kwa watu wote na hata milele. Kwa hiyo, wanangu, ishini uchangamfu, umakini, umoja na muwe na mapenzi baina yenu. Haya mnapaswa kuwa nayo katika ulimwengu wa leo: hivyo mtakuwa mitume wa upendo wangu, hivyo mtashuhudia Mwanangu kwa jinsi ya haki. Nawashukuru.
To compare Medjugorje messages with another language versions choose

 


Wap Home | Updates  | Medjugorje[EN]  | Messages  | News & Articles[EN]  | Videos[EN]  | Pictures & Photos[EN]

Powered by www.medjugorje.ws